Monday 11 November 2013

JINSI YA KUUNDA KIKUNDI CHA VICOBA

VICOBA (Village Community Bank) ni mfumo wa kuweka na kukopa kwa wanachama waliojiunga kwa pamoja na kuunda kikundi kwa malengo ya kujikwamua kiuchumi.

Mfumo huu ulianza Tanzania miaka kumi iliyopita na umeonyesha mafanikio makubwa kwa wanachama wake kuweza kukopeshana, kusaidiana katika matatizo mbalimbali, kuanzisha miradi ya pamoja ya kiuchumi.

MALENGO/MADHUMUNI YA KUUNDA VICOBA
Madhumuni ya kuunda vicoba ni kuunganisha nguvu na rasilimali za wanachama ili kuondoa umasikini na kuleta maendeleo kwa kufanya yafuatayo:-
  • Kuchangia/kununua hisa
  • Kuchangia mfuko wa jamii
  • Kuendesha mfuko wa kuweka na kukopa
  • Kushiriki katika mafunzo ya kuongeza ujuzi wa biashara, uongozi na uanzishaji wa shughuli mbalimbali za pamoja za maendeleo.
  • Kutafuata soko la pamoja na la uhakika kwa bidhaa za wanakikundi 

Kuna tofauti gani kati ya VICOBA na SACCOS?



VICOBA na SACCOS ni vikundi vya kiuchumi vyote vina malengo sawa isipokuwa mfumo wa uendeshaji.
  1.  Katika VICOBA wanachama uweka kiwango cha hisa na mara nyingi huanzia Sh.1000 na kuendelea, kiwango hicho ni kidogo ukilinganisha na kiwango cha hisa katika SACCOS.
  2.  WanaVICOBA umaliza mzunguko wao baada ya miezi kumi na mbili (12) na kufanya tathmini ikiwemo kugawana makusanyo na faida.
  3. Riba ya mkopo katika VICOBA ni ndogo (mara nyingi haizidi 10%)
  4. Kikundi cha VICOBA kinaundwa na wanachama 15-30, wanaoishi eneo moja au wanaofanya kazi pamoja.
  5.  Gharama za uendeshaji wa VICOBA ni ndogo kwani hakuna ofisi (wanachama huchagua mahali pa kukutana kwa muda usiozidi saa moja), vile vile viongozi wa VICOBA hawaajiriwi (wanafanya kazi za kujitolea)
VICOBA ikikuwa inaweza kuunda SACCOS. Mfumo wa Vicoba ni mzuri hasa kwa falsafa ya kuanza kidogo ili kuwa na kitu kikubwa hapo baadae. Licha ya kujihusisha na shughuri za kuweka na kukopa, wanavicoba husaidiana katika matatizo mbalimbali kama msiba na ugonjwa. Vile vile wanavicoba wanaweza kuanzisha mradi wa pamoja wa kikundi kwa kuunganisha rasirimali ndogo walizonazo. 
Hatua za Kuunda kikundi cha VICOBA
  1. Watu wenye wazo la kuanzisha kikundi kukutana (watu hao wasipungue kumi na tano na wasizidi thelathini)
  2. Wanachama kukusanya fedha za kiingilio (mara nyingi ni Sh. 10,000) kwa mwanachama. Fedha hiyo hutumika kununua vifaa kama leja,kasiki n.k. Fedha ya kiingilio vilevile hutumika kugharamia mafunzo ya awali na gharama ya usajili wa kikundi)
  3. Wanachama kuanza mafunzo yatakayosimamiwa na mwalimu mtaalamu wa mfumo huu wa vicoba.
  4. Wanachama kutunga katiba na sheria zitakayojumuisha kiwango cha hisa, mfuko wa jamii, siku ya kukutana n.k

Vicoba husajiliwa Brela kama jina la biashara (Business name) na kutambuliwa na halmashauri ya manispaa husika kupitia ofisi ya maendeleo ya jamii.
Mfumo huu ni rahisi kuuendesha na unamanufaa makubwa katika maendeleo ya kiuchumi. Ni fursa kwa vijana wenye mitaji midogo kuanzisha vikundi hivi ili kuunganisha rasirimali ndogo walizonazo na kwa pamoja kujiletea maendeleo.

9 comments: